Wednesday, April 18, 2012

USIPO ITAZAMA FURSA MUNGU ANAYOKUFUNGULIA KWA JICHO LA KIMUNGU NI RAHISI SANA KUJIKUTA UKIITUMIA VIBAYA,UKIIKATIA TAMAA NA HATA KUTOKUONA MANUFAA YAKE KATIKA MAISHA YAKO.


Mungu hafanyi mambo kwa hasara na ndio maana ili uone msaada wake unapoiendea fursa yoyote anayokufungulia katika maisha yako ni lazima ujifunze kuitazama fursa hiyo kwa jinsi ambayo yeye ameikusudia.Fursa yoyote Mungu anayoiachilia katika maisha ya mtu huwa ina kusudi maalumu. Na ndio maana kama usipoitazama kwa jicho la kimungu  ni rahisi sana ukajikuta ukiitumia vibaya,  au ukiikatia tamaa na hata kutokuona manufaa yake katika maisha yako.

Ukiitazama fursa yoyote Mungu anayoiachilia kwa jinsi ya kibinadamu ni vigumu sana kuona thamani ya kile kilichobebwa ndani ya hiyo fursa.Watu wengi wamejikuta wakichezea fursa Mungu anazowafungulia kutokana na kushindwa kuzitazama fursa hizo kwa jicho la kimungu.Wengi wamekuwa wakizitazama  kwa jicho la kibinadamu na hivyo kujikuta wakikatishwa tamaa na mazingira au changamoto wanazokutana nazo katika maisha yao.

Ukisoma katika Mwanzo 25:29-34, utaona jinsi gani Esau alivyoichezea fursa aliyopewa ya kuwa mzaliwa wa kwanza.Na kwa kutokujua thamani ya fursa ile alijikuta anaiuza kwa ndugu yake tena  kwa gharama ndogo ya chakula tu ili atulize njaa iliyokuwa ikimsumbua. Ukitafakari kwa undani utagundua tofauti kubwa kati ya  Esau na Yakobo hususani kwenye jinsi walivyokuwa wakiitazama fursa ya uzaliwa wa kwanza.Kila mmoja aliitazama kwa jinsi ya kwake,Esau aliitazama fursa ile kwa jicho la kibinadamu na ndio maana hakuona kile ambacho Yakobo alikiona.Yakobo aliuona uzaliwa wa kwanza kwa jicho la tofauti,alijua baraka zilizofungwa ndani ya nafasi ya mzaliwa wa kwanza na ndio maana Esau alipochezea fursa ile kwasababu ya njaa yake Yakobo aliichangamkia sawasawa bila kupoteza mda.

Macho ya ndani ya watu  yamekuwa na upofu kutokana na kutokukaa vizuri na Mungu.Na hii inapelekea wengi kushindwa kutazitazama fursa zinazofunguliwa katika maisha yao kwa jinsi Mungu anayotaka wazitazame. Watu wengi wamejikuta wakiuza fursa zinazofunguka maishani mwao kama Esau alivyouza uzaliwa wake wa kwanza tena bila kujua yakuwa wanachokiuza kinathamani kuu kiasi gani.Esau alikuwa na upofu kwenye macho yake ya rohoni na hivyo hakuona thamani ya uzaliwa wake wa kwanza na ndio maana haikumpa tabu kuiuza kwa ndugu yake Yakobo.Ukiitazama fursa kwa jicho la kibinadamu kama Esau, utajikuta ukiiona njaa zaidi kuliko uthamani na baraka zilizofungwa ndani ya uzaliwa wa kwanza ambazo zinaonwa kwa jinsi ya rohoni pekee.

Ni hasara kiasi gani kuuza fursa ambayo ingeweza kuamua hatima ya maisha yako kwasababu ya njaa ya kitambo tu.Leo tunao wakina Esau chungu mzima makanisani na majumbani mwetu, watu wako tayari kuuza wokovu wao kwasababu ya vitu vya kidunia.Fursa ya wokovu tuliyopewa tena kwa neema tunaishusha thamani, tunaiuza kama Esau alivyo uza uzaliwa wake wa kwanza kwasababu ya chakula ambacho ni chakupita tu.Leo hii utakuta mpendwa yuko tayari achezee wokovu wake na kuanguka dhambini kisa ni hofu ya kuchelewa kuolewa, eti umri umeenda anahofia atakimbiwa.Leo makanisa yamekuwa kama vitega uchumi,karama na neema Mungu anazoiachilia bure zinatumiwa kunufaisha matumbo ya watu na familia zao na si katika kuujenga mwili wa Kristo.

Ni muhimu kukumbuka kwamba Mungu anapoachilia fursa yoyote katika maisha yako lengo lake ni kukupeleka kwenye kiwango kingine cha maisha ambacho amekukusudia.Na hivyo haijalishi ni fursa ya namna gani Mungu anayokufungulia, kama usipoitazama fursa hiyo kwa jicho la kimungu basi ni dhahiri kwamba fursa hiyo haitofanyika msaada kwako.Maadamu umeiona fursa tofauti na makusudi ya Mungu basi uwe na uhakika hata utekelezaji au utumiaji wako wa fursa hiyo utakuwa nje ya utaratibu  Mungu aliyoukusudia wakati anaiachilia kwenye maisha yako.Kamwe usitegemee msaada wa Mungu katika fursa yoyote anayokufungulia kama unaiendea au unaitumia fursa hiyo nje ya makusudi ambayo kwayo alikufungulia.
Maombi yangu na dua yangu kwa Mungu, ni Mungu akatie nuru ndani ya macho ya moyo wako ili ukapate kuona fursa anazokufungulia kwa jinsi ambayo yeye ameikusudia.Shalooom!

Prepared by
MASSAWE GILBERT
SAA YA WOKOVU NI SASA

No comments:

Post a Comment